Bila shaka ni watu wengi wameshalisikia jina la Ken
Saro-Wiwa kutokana na umahiri wake wa kuandika riwaya lakini naamini pia kuna
wengi ambao hawamfahamu kiundani mwanaharakati huyu ambaye alipigania haki za
watu wa sehemu aliyokuwa anatokea ya Ogoni huko Nigeria ili ipate mgao sawa wa
pato la mafuta ambayo yalikuwa yanapatikanika katika eneo hilo lakini pia
alitaka kuhakikisha mazingira ya Ogoni yanalindwa dhidi ya uchafuzi uliokuwa
unafanywa na kampuni ya Shell.
Nyota ya mwanaharakati huyu wala haikudumu kwani
aliuwawa kwa kunyongwa kwa kile kilichosemekana kuwa alihusika katika mauaji ya
machifu wa Ogoni.
Binafsi naamini kuwa serikali ya kijeshi ya wakati huo ya
Nigeria na wale wote waliokuwa wanamampinga Saro-Wiwa walikuwa hawajamuelewa
hata kidogo kile ambacho alikuwa anakizungumza na mbaya zaidi walikuwa
wanafuata mkumbo wa watu ambao walikuwa na maslahi yao binafsi katika suala la
mafuta wakati huo.
Yaliyotokea Ogoni na Ken Saro-Wiwa sio kwamba yanafanana
na yale yanatokea Mtwara hivi sasa ila tu yanafafa kimahesabu na hasa katika njia zake za
kukokotoa japo hatuna uhakika na jibu litakuwa lipi.
Tumeshuhudia mwishoni kabisa mwaka jana wananchi wa Mtwara
wakiandamana kupinga kutoka Mtwara mjini mpaka eneo la Msimbati ambalo ndipo
gesi asilia inavunwa kupinga kusafirishwa kwa nishati hiyo mpaka jijini Dar es
Salaam.
Baada ya maandamano hayo ambayo yalionesha na kuwaamsha
wananchi wengi ndani na nje ya nchi msimamo wa watu wa Mtwara kwamba hawataki
gesi ipelekwe kwingine ndipo sasa kauli mbalimbali zikaanza kutolewa na
serikali ikionesha kusimamia msimamo wake wa kuendelea na mchakato wa
kusafirisha gesi hiyo kuja Dar es Salaam.
Binafsi sikuridhishwa maelezo aliyoyatoa Waziri wa Nishati
na Madini Professa Sospeter Muhongo ambaye naamini kabisa yeye ni msomi ndio
maana anaitwa Professa.
Jambo ambalo sikuelewa na wala sielewi mpaka sasa ni
kuhusiana na majibu aliyoyatoa Waziri kwa kuwapinga waziwazi tena bila kuuma
maneno wananchi wa Mtwara, sasa Je alikuwa anawapinga kisomi, kisiasa ama ni
kutokana na utashi wake mwenyewe kwani binafsi majibu aliyoyatoa naamini ndiyo
yamekuwa chimbuko ama chanzo cha vurugu, kurushiana maneno hata mie mwenyewe
kuandika hii makala na hata wewe msomaji kusoma makala hii.
Ki ukweli ni kwamba Mhe. Waziri alikosea, naamini kabisa
yeye pamoja na wenzake ambao wanawapinga wakazi wa Mtwara hawajawaelewa kabisa
nini wanachotaka.
Kama wanataka gesi ibaki Mtwara jibu ni rahisi tu,
wanaweza wakaiacha ibakie huko huko na inawezekana isiwanufaishe chochote
wakazi hao licha ya kwamba watakuwa wanaiona na kusikia ipo Msimbati.
kitu ambacho nasikiri ni kwamba, wananchi hawa wanataka
kuona ni jinsi gani gesi hii itaweza kubadilisha maisha yao ya kila siku tena
ya mwananchi wa hali ya chini kabisa. Hapa namaanisha upatikanaji wa huduma
muhimu za kijamii mfano afya, elimu, maji na mengineyo.
Tukumbuke kuwa wakazi hawa wanajua hali ikoje kwa watani
zao waliopo Geita, Kahama, Mwadui na kwingineko kwenye madini hivyo wanaogopa
kuishia mikono mitupu na kuendelea kuuza korosho ambazo nazo walitarajia kuinua
maisha yao lakini ndo hivyo ndoto zao zikaenda na maji kama machozi ya samaki
baharini.
Takwimu za elimu zinaonesha kuwa mikoa ya kusini mwa
Tanzania hususa Mtwara na Lindi ndiyo ambayo imekuwa ikishika nafasi za mwisho
katika matokeo mbalimbali ya elimu, kutokana na hilo wanafunzi wengi katika
mikoa hiyo wamekuwa wakikosa nafasi za kufika mbali kielimu mfano Chuo Kikuu na
hatimaye kujiajiri ama kuajiriwa ili kusaidia familia zao na jamii nzima
inayowazunguka.
Matokeo hayo mabaya yanadhirisha pia kuwa pengine hakuna
fungu zuri la fedha linaloelekezwa katika elimu katika mikoa hiyo hivyo kufanya
hali kuwa mbaya na mbaya zaidi mikoa ya kusini kuonekana ni mikoa ya kuzalisha
wafanyabiashara wadogo wadogo “machinga” na sio wasomi kama mikoa mingine.
Kama ningelikuwa mwanafunzi natakiwa nitoe jibu katika
hesabu hii, naona kuwa serikali inatakiwa kuhakikisha inaboresha kwanza miundo
mbinu ya mikoa ya kusini hususa mkoa wa Mtwara na Lindi, inaelekeza nguvu zaidi
katika elimu kwa kuboresha majengo, vifaa mpaka kupatika kwa walimu wenye uwezo
ambao watalipwa vizuri bila matatizo.
Kama hiyo haitoshi wakazi hawa wanataka kuhakikishiwa
usalama wa maisha yao na hapa nazungumzia afya, hospitali ambazo zina
wataalamu, vifaa na dawa za kutosha.
Pengine kwa kumalizia, ndugu zangu hawa wa Mtwara na
wengine kusini wangependa nao kuona vijana wao wanapata ajira katika makampuni
ama mashirika ambayo yanafunguliwa katika mikoa yao lakini sio tu kuona wageni
hususa kutoka nje ya nchi ndio wanaofaidika zaidi.
Kwa jibu hili la hesabu
naamini kabisa serikali itaweza kuwashawishi wakazi hao kusafirishwa kwa gesi
kwenda kwingine ili angalau nao walau wapate neema ambayo wao wanaipata kwani
Tanzania ni moja na itaendelea kuwa moja kwa amani na utulivu.
Anuary Mkama
0716-387577