Nchi
za Kusini mwa Jangwa la Sahara hatari kwa mtoto anayezaliwa- Taarifa ya Shirika
la Save the Children kuhusu Hali ya Wazazi Ulimwenguni - 2013
Save
the Children imezindua taarifa yake ya Hali ya Wazazi Ulimwenguni leo, 7 Mei,
2013 ikiwa na faharasa ya hatari ya kuzaliwa (Birthday Risk Index) ikionesha
kuwa nchi za Afrika, Kusini mwa Jangwa la Sahara zinabaki kuwa ukanda hatari
kwa mtoto anayezaliwa.
Katika
taarifa hiyo,Tanzania iko katika nafasi ya 10 miongoni mwa nchi zenye idadi
kubwa ya vifo vinavyotokea siku ya kwanza ya kuzaliwa ulimwenguni. Kiafrika
Tanzania ni nchi ya tatu kwa vifo
vinavyotokea siku ya kwanza ya kuzaliwa baada ya Nigeria na DRC na kwa
ukanda wa Afrika mashariki inaongoza. Vilevile, Tanzania inachangia asilimia 2%
ya vifo vinavyotokea siku ya kwanza ya kuzaliwa ulimwenguni, ambavyo huchangiwa
zaidi na matatizo ya uzazi kabla ya muda wa kujifungua, ukosefu wa vifaa vya
kujifungulia, na changamoto za kupata huduma kwa watoto wachanga, hususani kwa
kina mama wanaoishi maeneo ya vijijini.
Tanzania imefanya mabadiliko makubwa ya kisera katika kupanua
huduma za afya kwa watoto wanaozaliwa. Pamoja na hilo, kwa mujibu wa taarifa
hii, watoto 17,000 hufa katika siku zao za kwanza za kuzaliwa na pia watoto
48,000 hufa kila mwaka, hivyo kuiweka Tanzania miongoni mwa nchi 10
zinazoongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya vifo vya watoto wach
anga,” anasema Dk.
Stephen Ayella, Mshauri wa Programu ya Afya wa Save the Children nchini
Tanzania.
Somalia,
Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo (DRC), Mali, Sierra Leone, zina idadi kubwa
zaidi ya vifo vya watoto wachanga ulimwenguni. Mathalani, kwa mujibu wa taarifa
hiyo, nchini Somalia, mtoto anayezaliwa yuko katika hatari ya kufa mara 40
zaidi kuliko mtoto aliyezaliwa Luxembourg. Vifo vya watoto wachanga, hususani
katika siku ya kwanza ya kuzaliwa ni ishara hali ya usalama wa wazazi kutokana
na matatizo ya wakati wa kujifungua na hali ya mtoto mchanga ndani ya masaa 24
baada ya kuzaliwa.
Ulimwenguni
kote, watoto milioni moja hufa kila mwaka katika siku yao ya kwanza ya kuzaliwa
ama kwa lugha nyingine watoto wawili hufa kila dakika, hivyo kuifanya siku ya
kwanza kuwa siku ya hatari zaidi kwa maisha ya mtu karibu katika kila nchi
ulimwenguni.
Takwimu
za kitaifa zilizotolewa katika faharasa zinaangazia nchi nyingi ulimwenguni.
Viashiria kama hatari za vifo wakati wa uzazi, vifo vya watoto chini ya miaka
5, idadi itarajiwayo ya miaka ya mahudhurio katika shule rasmi, pato la taifa
na ushiriki wa wanawake katika uongozi wa serikali vimetumika katika kupanga
nafasi. Kati ya nchi 176 ulimwenguni, Tanzania ni nchi ya 135, ikionesha
kupanda kidogo ukilinganisha na mwaka jana ambapo ilishika nafasi ya 140.
Taarifa
imebainisha mambo ya msingi yanayochangia katika idadi hiyo kubwa barani
Afrika. Mambo hayo ni pamoja na idadi kubwa ya watoto wanaozaliwa kabla ya
kutimiza muda, kama ilivyo katika mfano wa Malawi ambayo ina idadi kubwa ya
watoto wanaozaliwa kabla ya kutimiza muda na ambao wanazaliwa na uzito pungufu.
Mambo mengine ni pamoja na afya duni za wazazi, uzazi katika umri mdogo,
ambavyo vinawaweka wazazi katika hatari ya kupata matatizo wakati ya uzazi
yakiwa ni pamoja na mtoto aliye tumboni kutokuwa katika kiwango kinachostahili
na kuzaa kabla ya muda.
Mkurugenzi wa
Save the Children wa Ukanda wa Afrika Magharibi na Kati, Natasha Quist, anasema:
“Nchi za Afrika na jumuiya ya ulimwengu wanafanya juhudi za kumaliza vifo vya
watoto vinavyoweza kuzuilika, hata hivyo kama tunataka kufikia lengo hili la
kihistoria, kunahitajika juhudi za ziada kuelekezwa katika kunusuru maisha ya
watoto katika siku na miezi yao ya kwanza ya kuzaliwa.”
Wataalam wa
masuala ya watoto wachanga wanakiri kuwa maendeleo makubwa yangeweza kufanyika
kwa kueneza mbinu rahisi, zenye tija na gharama ndogo na kubadilishana mifano
bora katika bara hilo.
Kupitia miradi
yake ya Kuokoa Maisha ya Watoto Wachanga (SNL) na MAISHA, Save the Children nchini Tanzania imekuwa mstari wa mbele nchini
katika kuanzisha na kufuatilia huduma za Malezi kwa Mtindo wa Kangaroo (KMC),
mtindo ambao ni maalum kwa kutunza watoto njiti na wenye uzito pungufu. Kwa
kushirikiana na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Save the Children imeanzisha
vituo 27 vya Malezi ya Mtindo wa Kangaroo Tanzania bara na Visiwani. Pia
imefundisha zaidi ya wauguzi na madaktari 973 pamoja na kuwaelekeza juu ya
Mtindo wa Kangaroo wafanyakazi 1185 wa kada zingine za afya.
Save the
Children inakadiria kuwa maisha ya watoto wachanga milioni moja yanaweza
kuokolewa kila mwaka, kuhakikisha upatikanaji wa vitu vinne tu ambavyo gharama
yake ni ndogo: sindano za Corticosteroid kwa kina
mama walio katika uchungu wa kabla ya muda, ambazo ni muhimu katika kupunguza
vifo vitokanavyo na matatizo ya kupumua kwa watoto wanaozaliwa; vifaa vya
kuamsha watoto wanaoshindwa kupumua baada ya kuzaliwa; dawa ya kusafishia baada
ya kondo kutoka ili kuzuia maambukizi yanayotokana na kondo la nyuma na madawa
ya sindano za kuzuia matatizo ya kuvimba
na kifua kwa watoto.
Vilevile,
katika taarifa hiyo, Save the Children inaendelea kuonesha uhusiano kati ya
afya ya mama mjamzito na vifo vya watoto wachanga. Faharasa hiyo ya Hali ya
Wazazi Ulimwenguni inapanga huduma ambazo kila nchi inazitoa kwa kina mama
kulingana na viashiria vya afya ya mama mjamzito, watoto chini ya miaka mitano,
kiwango cha elimu kwa kina mama, kipato na hali ya kisiasa. Finland inaongoza
ambapo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo inashika mkia.
Save
the Children inatoa wito ufuatao kwa viongozi ulimwenguni:
§ Kuwekeza katika mambo yenye gharama
nafuu na ambayo yanaweza kupunguza kwa kiasi kikubwa vifo vya watoto wachanga. Madawa
yanayoweza kutibu ama kuzuia maambukizi madogo madogo ambayo yanaweza
kusababisha vifo. Vilevile kuhimiza unyonyeshaji wa maziwa ya mama pekee na malezi
ya Mtindo wa Kangaroo, mambo ambayo hayana gharama yoyote, lakini yanaweza
kuokoa maisha ya maelfu ya watoto.Vilevile, wahudumu wa kina mama wanaojifungua
wanapaswa kupewa mafunzo, msaada na vifaa vya kutosha ili waweze kutoa huduma
kwa ufasaha.
§ Kuimarisha mifumo ya afya ili kina mama wengi zaidi waweze
kufikiwa na wahudumu wa afya wenye ujuzi. Kuwekeza zaidi katika wahudumu wanaopokea wagonjwa
na wahudumu wa afya katika jamii ili kuweza kusaidia kuwafikia kina mama na
watoto walio katika hatari zaidi.
.
§ Kupambana na viini vya
vifo vya watoto wachanga, usawa wa kijinsia na utapiamlo. Kusaidia kina mama kuwa na nguvu na imara-kimwili, kifedha na
kijamii kunasaidia kuwawezesha watoto wao pia kuwa na nguvu na kuweza kuishi na
kukua.
Dk.
Rachel Makunde, Meneja Programu ya Afya ya Mama Wajawazito na Watoto wa Save
the Children nchini Tanzania anatoa wito kwa serikali kuelekeza nguvu zaidi
katika mipango na bajeti kwa ajili ya kuokoa maisha ya watoto, ikiwa ni pamoja
na kueneza huduma ya Malezi kwa Mtindo wa Kangaroo hadi hospitali za wilaya na
katika vituo vya afya.
“Kuzaliwa kabla ya muda kunachangia vifo vya watoto wachanga kwa
asilimia 35, kwa hivyo afua zenye kulenga watoto njiti zinaweza kuchangia kwa
kiasi kikubwa kupunguza vifo vya watoto,” anasema.