Karibu katika blog yetu

Tuesday, May 28, 2013

Kongo yagawika pendekezo la Rais Kikwete


Pendekezo la Rais Jakaya Kikwete wa Tanzania kwa serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo izungumze na makundi ya waasi na nchi jirani kutatua mzozo wa mashariki ya nchi hiyo linaonekana kuwagawa Wakongo.
Kwenye mji mkuu wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Kinshasa, kuna mwangwi wa sauti za Wakongomani wakiupongeza msimamo wa Rais Kikwete kwamba kuweko na mtazamo wa ujumla katika kutafuta ufumbuzi wa mzozo wa kanda ya Maziwa Makuu.
Mwandishi wetu wa Kinshasa anaripoti kwamba wakaazi wengi wa mji huo wanaamini kuwa pendekezo hilo la Rais Kikwete linaweza kusaidia amani ya kudumu.
Kwenye mkutano wa marais 11 wa Nchi za Maziwa Makuu kwa ajili ya Kongo uliotishwa kando ya mkutano wa Umoja wa Afrika, mjini AddisAbaba, Rais Kikwete alipendekeza kufanyike mazungumzo baina ya Kongo na kundi la waasi la M23, Rwanda na kundi la waasi la FDLR na Uganda na waasi wake wa ADF/Nalu kwa ajili ya amani ya kudumu ya kanda ya Maziwa Makuu.
Tanzania inachangia wanajeshi 1,280 kwenye kikosi maalum cha Umoja wa Mataifa mashariki mwa Kongo,
Umoja usio wa kawaida Kinshasa
Rais Paul Kagame wa Rwanda (kushoto) na Joseph Kabila wa DRC.Rais Paul Kagame wa Rwanda (kushoto) na Joseph Kabila wa DRC.
Pendekezo hili limezua kile mwandishi wetu wa Kinshasa anachokiita “tukio la nadra kabisa nchini Kongo“ kwa wabunge wa upinzani na wale wa chama tawala kuwa na kauli moja kuhusu maswala muhimu ya kitaifa.
Rais Kikwete amefanikiwa kuwaelekeza wanasiasa wa Kongo kuchukuwa msimamo wa pamoja kuhusu juhudi za kutafuta suluhisho la kudumu kwenye kanda ya Maziwa Makuu.
Kwa mujibu wa taarifa za mashirika ya habari ni kwamba Rais Kikwete aliwambia maraisi wenzake pamoja na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon, na Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika Afrika, kwamba ni lazima kuweko na mtizamo wa ujumla kwa ajili ya kumalizisha machafuko ya miaka mingi kwenye kanda la Maziwa Makuu.
Kwa hiyo Rais Kikwete alipendekeza Kongo kuendesha mazungumzo na waasi wa M23, na vilevile kuitaka Rwanda kuzungumza na waasi wa FDLR na Uganda kufungua mazungumzo na waasi wake wa ADF/Nalu. Pendekezo hilo limepongezwa na upinzani na chama tawala nchini Kongo, akiwemo mbunge Justin Bitakwira, ambaye ni kiongozi wa wabunge wa upinzani wa UNC.
Naye Franklin Tshamala, msemaji wa muungano wa vyama tawala, amesema kwamba pendekezo hilo la Rais Kikwete ni hatua ya ujasiri ya kutaka kurekebisha mitizamo tofauti waliyonayo viongozi wa mataifa haya matatu.
Rwanda yakataa
Wanajeshi wa Umoja wa Mataifa nchini DRC.Wanajeshi wa Umoja wa Mataifa nchini DRC.
Pendekezo hilo la Rais wa Tanzania lilipongezwa pia na serikali ya Kongo. Akiwa mjini Addis Ababa, Waziri wa Mambo ya Nje ya Kongo, Raymond Tshibanda, aliiambia Radio France Internationale kwamba msimamo huo unalingana na ombi la miaka mingi la serikali ya Kongo kwa majirani zake.
Lakini Waziri wa Mambo ya Nje wa Rwanda, Louise Mushikiwabo, aliyehojiwa na redio hiyo hiyo alisema matamshi hayo ya Rais Kikwete ni ya upotofu na nchi yake haiwezi kamwe kuzungumza na watu waliohusika na mauwaji ya halaiki.
Magazeti mengi ya siku ya Jumanne (tarehe 28 Mei) yamezungumzia matamshi ya Rais Kikwete na maoni ya wananchi wa Kongo. Gazeti Lavenir limechapisha kichwa cha habari kwa wino mzito kikimuita Rais Kikwete ”Jjasiri wa kanda ya Maziwa Makuu.”
Kwenye ukarasa wa mwanzo, gazeti la upinzani la Tempetes des Tropiques limeandika “Kikwete arusha bomu Addis Abeba”, likiyaelezea matamshi ya Rais Kikwete kuwa sawa na bomu alilowarushia marais wenzake ambao kwa muda mrefu wameonyesha unafiki katika kumaliza machafuko ya Maziwa Makuu kwa zaidi ya miaka 20 sasa.
Goma hawataki mazungumzo na M23
Wakimbizi wa ndani mashariki ya Kongo.Wakimbizi wa ndani mashariki ya Kongo.
Lakini hali ikiwa hivyo mjini Kinshasa, kwenye eneo la mashariki ya Kongo, ambako ndiko hasa kwenye mgogoro kati ya serikali na waasi wa M23, maoni ni tafauti.
Mwandishi wetu wa Goma, John Kanyunyu, anaripoti kwamba mashirika ya kiraia ya huko yamekataa mazungumzo baina ya serikali ya DRC na wajumbe wa M23.

Makamu mwenyekiti wa mashirika ya hayo kiraia katika mkoa wa Kivu ya Kaskazini, ambaye pia ni msemaji wa mashirika hayo, Omar Kavota, amesema “hakuna tena la kuzungumza, kwani tayari mkataba wa M23 baina ya chama cha zamani cha uasi CNDP umeshajadiliwa.”

Kauli hiyo ya mashirika ya kiraia inakuja baada ya pendekezo la Rais Kikwete mbele ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa na marais wa kanda ya Maziwa Makuu kuiomba serikali kurudi kwenye meza ya mazungumzo baina yake na waasi wa M23.
Aidha kauli hiyo ya mashirika ya kiraia ya kuitaka serikali kutozungumza na wajumbe wa M23, inachochewa pia na utendaji kazi wa wanajeshi wa serikali katika uwanja wa mapigano.

Katika vita baina ya jeshi la serikali, FARDC, na waasi wa M23, jeshi hilo la serikali linatajwa kuwa, lilifaulu kwa mara ya kwanza kabisa, kuwazuia waasi wa M23 kuuteka upya mji wa Goma.

Kavota anasema ni bora zaidi kuwapatia nafasi ya kufanya kazi zao wanajeshi wa kikosi maalumu cha Umoja wa Mataifa kinachowajumuisha wanajeshi kutoka Tanzania, Malawi na Afrika ya Kusini.
Katika kuwapongeza wanajeshi wa serikali kwa kazi waliyoifanya wakati wa mapigano ya wiki iliyopita, mashirika ya wanawake kutoka asasi za kiraia na vyama vya kisiasa, wametoa mchango wa pesa wa kile walichokiita “kuwanunulia wanajeshi wa serikali maji ya kunywa.”
Ripoti hii imetayarishwa na Saleh Mwanamilongo, Kinshasa, na John Kanyunyu, Goma
Mhariri: Mohammed Khelef

Friday, April 19, 2013

KUTOKA TFF


MECHI YA MGAMBO, YANGA YAINGIZA MIL 24/-
Mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom kati ya Mgambo Shooting na Yanga iliyochezwa jana (Aprili 17 mwaka huu) Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga imeingiza sh. 24,865,000 kutokana na watazamaji 4,386.

Viingilio katika mechi hiyo namba 162 iliyomalizika kwa timu hizo kutoka sare ya bao 1-1 vilikuwa sh. 10,000 kwa jukwaa kuu na sh. 5,000 huku kila klabu ikipata mgawo wa sh. 5,547,337.50 wakati Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) iliyolipwa ni sh. 3,792,966.10.

Asilimia 15 ya uwanja sh. 2,820,680.08, msimamizi wa kituo sh. 120,000, kamishna wa mechi sh. 90,000, waamuzi sh. 270,000, maandalizi ya uwanja sh. 100,000 na tiketi sh. 1,587,500.

Mgawo mwingine ni gharama za mechi sh. 1,692,408.05, Kamati ya Ligi sh. 1,692,408.05, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 846,204.05 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Tanga (TRFA) sh. 658,158.69.

MAKOCHA AZAM, FAR RABAT KUTETA
Makocha wa timu za Azam, Stewart John Hall na AS FAR Rabat ya Morocco, Abderazzak Khairi watakutana na waandishi wa habari kesho (Aprili 19 mwaka huu) kuzungumzia mechi yao itakayofanyika Jumamosi, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Mkutano huo ambao pia utawahusisha manahodha wa timu hizo mbili utafanyika saa 5 kamili asubuhi kwenye ofisi za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) zilizoko Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Barabara ya Uhuru na Shaurimoyo.

Timu hizo zitakutana katika mechi hiyo ya kwanza ya raundi ya pili ya Kombe la Shirikisho itakayoanza saa 10 kamili jioni. Mechi ya marudiano itachezwa nchini Morocco wiki mbili baadaye.

JKT RUVU, YANGA KUUMANA JUMAPILI
Yanga ambayo inafukuzia kwa karibu taji la Ligi Kuu ya Vodacom itapambana na JKT Ruvu katika mechi pekee ya ligi hiyo wikiendi hii itakayofanyika Jumapili (Aprili 21 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Mbali ya mechi hiyo, nyingine zitakazochezwa mwezi huu ni kati ya African Lyon na JKT Ruvu itakayofanyika Aprili 24 kwenye Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam wakati Aprili 25 ni kati ya Ruvu Shooting na Simba kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Nayo Coastal Union itaikaribisha Azam kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga katika mechi itakayochezwa Aprili 27. Uwanja wa Taifa utakuwa mwenyeji wa mechi kati ya Simba na Polisi Morogoro itakayofanyika Aprili 28.

Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

Thursday, April 11, 2013

WALIMU WAPINGA MPANGO WA SERIKALI KUSHUSHA ALAMA ZA UFAULU

Kufuatia kauli ya Naibu Waziri wa Elimu na mafunzo ya ufundi Philipo Mulugo kusema kuwa serikali inakusudia kushusha alama za ufaulu kwa wanafunzi wa kidato cha nne kuelekea kidato cha tano na cha sita, wananchi pamoja na baadhi ya walimu ambao hawakupenda kutajwa majina yao wamesema kuwa njia hiyo sio suluhisho la kuinua elimu nchini bali kuzidi kudidimiza.

Wakiongea mjini hapa Kigoma, wamesema kushusha huko alama kutakuwa kunamfurahisha mwanafunzi na wazazi wake katika makaratasi huku mwanafunzi huyo kichwani hakiwa hajaelimika vya kutosha.

Wameongeza na kusema serikali inatakiwa kuhakikisha inatafutia ufumbuzi wa kudumu matatizo ya elimu yaliyopo kama nyezo za kufundishia, kuongeza idadi ya walimu sanjari na mishahara pamoja na ujenzi wa nyumba zao.

Akiongea katika mkutano na wamiliki wa shule za sekondari nchini uliofanyika mjini Mbeya, Naibu waziri Mulugo amesema kuwa mpango huo wa kushusha alama ya ufaulu kwa kidato cha nne utasaidia kutoa nafasi zaidi kwa wanafunzi kupata nafasi ya kusoma kidato cha tano na cha sita.

KOCHA RHINO APIGWA FAINI, AFUNGIWA MECHI SITA


KAMATI ya Ligi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imempiga faini ya sh. 400,000 na kumfungia mechi sita Kocha wa Rhino Rangers, Renatus Shija kwa kushiriki vitendo vinavyoashiria imani za ushirikina na kumdhihaki mwamuzi kwenye mechi za Ligi Daraja la Kwanza (FDL).

Adhabu hizo zimetolewa kwa mujibu wa kifungu cha 31(1)(a) na (b) cha Kanuni za FDL ambapo Kocha huyo aliyeipandisha daraja Rhino Rangers kucheza Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) alifanya vitendo hivyo kwenye mechi mbili tofauti.

Mechi hizo ni kati ya Kanembwa JKT na Rhino Rangers iliyochezwa Februari 23 mwaka huu Uwanja wa Lake Tanganyika mjini Kigoma, na ile kati ya Rhino Rangers na Morani iliyochezwa Machi 17 mwaka huu Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora.

Pia klabu ya Rhino Rangers imepigwa faini ya sh. 200,000 kutokana na Polisi Wanajeshi- MP kuwapiga walinzi milangoni kwenye mechi hiyo dhidi ya Kanembwa JKT ili kupisha washabiki wa timu hiyo waingie bure uwanjani.

Mchezaji wa timu ya Pamba ya Mwanza, Leonard Nahole amepigwa faini ya sh. 200,000 na kufungiwa mechi nne baada ya kumrushia chupa ya maji mwamuzi kwa madai amependelea kwenye mechi dhidi ya Polisi Tabora iliyochezwa Machi 16 mwaka huu.

Nao wachezaji Joseph Mapalala, Yohana Mirobo, Noel Makunja, Mkome Pastory na Rudenzi Kilinga wa Polisi Mara wamepigwa faini ya sh. 200,000 kila mmoja na kufungiwa mechi tatu kwa kufanya vitendo vinavyoshiria ushirikina na kumkimbiza mwamuzi kwenye mechi dhidi ya Morani iliyochezwa Machi 9 mwaka huu. Adhabu za wachezaji hao ni kwa mujibu wa kifungu cha 27(1)(g) cha Kanuni za FDL.

Klabu ya Villa Squad imepigwa faini ya sh. 150,000 kwa kuchelewa uwanjani kwenye mechi yake dhidi ya Ashanti United wakati Majimaji imepigwa faini ya sh. 200,000 kutokana na washabiki wake kufanya vurugu kwenye mechi dhidi ya Mbeya City iliyochezwa Uwanja wa Majimaji.

Vilevile Msimamizi wa Uwanja wa Majimaji aliyetambulika kwa jina moja la Mapunda aliwatukana waamuzi kwenye mechi hiyo, na suala lake litafikishwa kwenye Kamati ya Nidhamu ya TFF kwa ajili ya hatua za kinidhamu.

Pia uongozi wa Uwanja wa Mafinga unaotumiwa na timu ya daraja la kwanza ya Kurugenzi umetakiwa kuufanyia marekebisho, vinginevyo hautatumika kwa mechi za FDL msimu ujao.

Tuesday, April 9, 2013

MLIMANI TV KATIKA

Kigoma yakabiliwa na uhaba wa walimu wa sayansi.

Imeelezwa kuwa mkoa wa Kigoma unakabiliwa na upungufu mkubwa wa walimu wa somo la sayansi hali ambayo inachangia kwa kiasi kikubwa wanafunzi wa kidato cha nne na sita kushindwa kufanya vizuri katika mitihani yao ya taifa.

kauli hiyo imetolewa na Afisa elimu msaidizi wa Kigoma bwana Venance Babukege wakati akizungumzia maendeleo ya elimu ya mkoa huo.

Bwana Babukege amesema idadi wa walimu wa masomo ya sanaa inaridhisha huku upande wa sayansi hali ni mbaya zaidi hivyo kusababisha wanafunzi wengi wasichague michepuo ya masomo hayo huku wale waliochagua nao wakipata matokeo ambayo hayaridhishi.

kwa upande wa walimu wanaofundisha masomo ya sayansi, babukege amesema wamekuwa wakiomba uhamisho pindi wanapopangiwa kigoma kutokana na kukosekanika nyenzo za kufundishia kwa vitendo.

katika mipango ya kujipanga kuhakikisha kiwango cha ufaulu kinaongezeka hususa kwa wanafunzi wa kidato cha nne mwaka huu, Babukege amesema kuwa hivi sasa kitengo chake kinatembelea katika shule zote za sekondari za mkoa kuzungumza na walimu ili kupata njia ambazo zitasaidia kuinua kiwango cha ufaulu.

Anuary- Kigoma.

Monday, April 8, 2013

TABORA NA MASOMO YA JIONI KWA KIDATO CHA NNE

Mkoa wa Tabora umeamua kutoa nafasi za masomo ya jioni kwa wanafunzi waliofeli kidato cha nne hivi karibuni ili kuwapa nafasi waweze kusawazisha makosa yao na hatimaye waendelee na masomo ya ngazi ya juu.
Afisa elimu wa mkoa huo Midamo Paul Makungu amesema kuwa ofisi yake imeshakubaliana na walimu wa shule za sekondari kuanzisha masomo hayo kwa wanafunzi watakaopenda.

Monday, March 25, 2013

Dk. Ali Mohamed Shein akutana na Mhe. Xi

   
RAIS wa  Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amefanya mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Watu wa China Mhe. Xi Jinping na kumueleza kuwa Zanzibar imefungua milango ya uwekezaji hivyo China inaweza kutumia fursa hiyo kwa kuekeza katika sekta mbali mbali za kimaendeleo.
 
Dk. Shein aliyasema hay leo wakati alipokuwa na mazungumzo na Rais wa China Mhe. Xi Jinping huko katika ukumbi wa hoteli ya Serena Jijini Dar-es-Salaam.
 
Katika maelezo yake Dk. Shein alimueleza Rais Xi  Jinping kuwa Tanzania ikiwemo Zanzibar inathamini uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya pande mbili hizo na kusisitiza kuwa ziara yake hiyo itakuwa ni fursa ya pekee ya kuweza kuitangaza Zanzibar katika sekta ya uwekezaji ili Zanzibar nayo inufaike.
 
Alisema kuwa Zanzibar imeweka mazingira mazuri ya uwekezaji hivyo inaikaribisha China  kuja kuekeza Zanzibar kwa lengo la kuzidi  kuimarisha uhusiano wa kidugu na wa kihistoria uliopo kati ya pande mbili hizo.
 
Dk. Shein alitoa shukurani na pongezi kwa China kutokana na kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika sekta mbali mbali za kimaendeleo kwa kutambua mchango wake mkubwa hasa ikizingatiwa kuwa China ni miongoni mwa nchi za mwanzo  zilizotambua Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964.
 
Alisema kuwa China imeweza kuunga mkono sekta mbali mbali za maendeleo na kusifu kazi nzuri inayofanywa na madaktari wa nchi hiyo ambao wanafanya kazi zao katika hospitali za Zanzibar pamoja na kusifu mchango wa nchi hiyo katika ujenzi wa hospitali ya Abdala Mzee kisiwani Pemba.
 
Dk. Shein alieleza kuwa China imeweza kusaida miradi mbali mbali ikiwa ni pamoja na kuipatia Zanzibar mikopo nafuu katika kuendeleza miradi ukiwemo mradi wa  maji safi na salama mnamo miaka ya 70, misaada katika sekta ya habari, nafasi za masomo, afya, miundombinu, ujenzi wa jengo la abiria la uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Karume unaoendelea, mawasiliano na miradi mengineyo.

Stars yamuweka matatani Taoussi

Majaliwa ya kocha mkuu wa Morocco Rachid Taoussi kuendelea kuifundisha timu ya taifa ya nchi hiyo yapo mashakani baada ya wadau wa soka wa Morocco kutaka kocha huyo ajiuzuru kutokana na kufungwa goli 3-1 na Tanzania katika mchezo wa kuwania kucheza kombe la dunia mwaka 2014 nchini Brazil.

Wadau hao wa soka nchini humo wamesema kuwa kocha huyo ameshindwa kuiletea timu yao mafanikio lakini wameponda pia kitendo chake cha kufanya mabadiliko makubwa katika kikosi kilichocheza katika michuano ya kombe la Mataifa ya Afrika na kile kilichopata kipigo cha aibu kutoka kwa Tanzania.

Morocco sasa inahitaji miujiza ili isonge mbele katika hatua nyingine ya kuwania nafasi ya kucheza fainali zijazo za dunia nchini Brazil.